Masomo ya Misa
Kumbukumbu ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa (Jumatatu, Mei 25, 2026)
Mwa 3:9-15, 20
Baada ya Adamu kule tunda la ule mti, Bwana Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi? Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha. Akasema, Ni nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je! Umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale? Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala. Bwana Mungu akamwambia mwanamke, Nini hili ulilolifanya? Mwanamke akasema, Nyoka alinidanganya, nikala. Bwana Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu umeyafanya hayo, umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote walioko mwituni; kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako; nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino. Adamu akamwita mkewe jina lake Hawa; kwa kuwa yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai.
1 Sam: 2:1, 4-8
Naye Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana,
Pembe yangu imetukuka katika Bwana,
Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu;
Kwa kuwa naufurahia wokovu wako;
(K) Moyo wangu wamshangilia Bwana mwokozi wangu.
Pinde zao mashujaa zimevunjika, Na hao waliojikwaa wamefungiwa nguvu.
Walioshiba wamejikodisha ili kupata chakula,
Na hao waliokuwa na njaa wamepata raha.
Naam, huyo aliyekua tasa amezaa watoto saba,
Na yeye aliye na wana wengi amedhoofika.
(K) Moyo wangu wamshangilia Bwana mwokozi wangu.
Bwana huua, naye hufanya kuwa hai;
Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu.
Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha;
Hushusha chini, tena huinua juu.
(K) Moyo wangu wamshangilia Bwana mwokozi wangu.
Humwinua mnyonge kutoka mavumbini,
Humpandisha mhitaji kutoka jaani,
Ili awaketishe pamoja na wakuu,
Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu;
Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana,
Naye ameuweka ulimwengu juu yake.
(K) Moyo wangu wamshangilia Bwana mwokozi wangu.
Lk 1:28
Aleluya, aleluya,
Salamu, Mariamu, ulipewa neema. Bwana yu pamoja nawe! Umebarikiwa katika wanawake.
Aleluya.
Yn 19:25-34
Penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake. Baada ya hayo Yesu, hali akijua ya kuwa yote yamekwisha kumalizika ili andiko litimizwe, akasema, Naona kiu. Kulikuwako huko chombo kimejaa siki; basi wakatia sifongo iliyojaa siki juu ya ufito wa hisopo, wakampelekea kinywani. Basi Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, Imekwisha. Akainama kichwa, akaisalimu roho yake. Basi Wayahudi, kwa sababu ni Maandalio, miili isikae juu ya misalaba siku ya sabato, (maana sabato ile ilikuwa siku kubwa), walimwomba Pilato miguu yao ivunjwe, wakaondolewe. Basi askari wakaenda, wakamvunja miguu wa kwanza, na wa pili, aliyesulibiwa pamoja naye. Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu; lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji.

Maoni
Ingia utoe maoni